Tuesday, October 8, 2013

Ndoa na Uaminifu


Uaminifu ndani ya ndoa hujenga familia bora!!! Yes tumekutana tena kwenye kona hii ya
Mapenzi na Uhusiano.
Kama inavyojulikana wazazi wawili ndiyo muongozo
wa familia, baba akiwa kichwa cha familia akifuatiwa
na mama. Siku zote familia bora hutegemea
muongozo mwema wa wazazi, kwani wao ndiyo walimu wa kwanza kwa mtoto. Siku zote watoto hujifunza kupitia wazazi wao
wanachokifanya ili nao wakitumie kama dira ya
maisha yao pindi wakifikia umri wa kujenga familia
zao. Kama muongozo utakaowafanya waweze
kuishi muda mrefu katika maisha ya ndoa na kifo
pekee ndicho kitakacho watenganisha. Katika maisha ya kila siku ya mwanadamu
hawawezi kuishi kama malaika, ipo siku wanaweza
kukosana kwani makosa ni sehemu ya maisha ya
mwanadamu. Ndiyo maana tumefundishwa
kusamehe au kuomba msamaha pale unapojua
umekosa. Lakini kuna baadhi ya familia zimekuwa
zikiwashirikisha watoto wao katika matatizo yao
pindi wakosanapo, ikiwamo kufokeana mbele yao
pindi wazazi wanapo tibuana. Mnashindwa kutafuta sehemu ya faragha na
kuonyana kiutu uzima, kama wazazi ambao siku
zote watoto hutakiwa kujifunza mazuri kutoka
kwenu. Kufokeana mbele ya watoto mnawafundisha
nini? Inapotokea baba au mama anapokuwa akimtumia
mtoto wake kujua kama mwenzake kuna kitu kibaya
amefanya kwa kumuuliza: “Ulipotembea na baba
yako hakuzungumza na wanawake?” Au baba
kukuuliza “Nilipokwenda kazini mama yako alitoka
au alizungumza na mwanamume?” Nina imani kwa mawazo yenu unajiona mpo sawa
kumbe sivyo, kwa mtindo huu inaonyesha ndani ya
uhusiano wenu hakuna uaminifu. Hamuwezi
kumfanya mtoto kama mlinzi wa mmoja wenu. Hivi
mnamfundisha nini au ndiyo mnajionyesha jinsi gani
msivyo aminiana. Kwani mtoto huamini matatizo ndani ya familia ni
msiba mzito ambao mwisho wake ni wazazi
kutengana na kuweka mpasuko katika maisha yake.
Mzazi mwenye busara siku zote hukanyana sehemu
ya faragha ambayo humfanya mtoto aamini siku
zote wazazi wake hawana matatizo. Pia kama una wasiwasi na mwenendo wa
mwenzako kwa nini usimwite mkae chini na kutatua
kwa busara, kwani hakuna mwanadamu
aliyekamilika asilimia mia. Familia bora ni ile ambaye inahakikisha matatizo
yao hayaathiri watoto wao, hutatua kwa busara huku
wakizingatia watoto wao wanawategemea wao.
Wazazi kuweni walimu wema katika familia zenu ili
kujenga familia yenye maadili mema.

No comments:

Post a Comment